A person who knows and is aware that he knows, is wise, follow him; A person who knows but is not aware that he knows, remind him; A person who doesn't know and is aware that he doesn't know, teach him; A person who doesn't know and pretends to know, is fool, leave him


Bless me in my undertakings Dear God, grant me victory and I shall shout your blessings for all to hear of your power!

Thursday, April 29, 2010

Nini thamani ya mwalimu wa Tanzania?

Kwa wale wanaopenda kusoma vitabu au maandiko kuhusu ualimu au mageuzi ya elimu duniani, wanaweza kuwa wanamfahamu mwandishi maarufu duniani wa mambo ya elimu na ualimu anayeitwa Michael Fullan, huyu bwana anaheshimika kimataifa kutokana na misimamo yake juu ya mabadiliko na maendeleo ya elimu duniani. Fullan anaamini kwamba mabadiliko ya kweli na ya haraka katika elimu yanaletwa na walimu. "Education change depends on what teachers think and do, it is as simple and complex as that"

Kuna waandishi wengine wengi kutoka nchi kama vile Japan, Marekani, Australia, New Zealand, Finland na Uholanzi walioandika mengi kuhusu namna walimu wanavyochangia kiasi kikubwa cha maendeleo ya elimu. Maandiko na tafiti hizi zimewaongezea heshima sana walimu mahali pengi duniani isipokuwa Tanzania. Na isitoshe kwa nchi kama Japan, mwalimu anapewa heshima ya ziada na watu wote, tangu wazazi, viongozi na wengineo. Kwa heshima hii, walimu hawa wanafanya kazi kubwa sana ya kusaidia kubadili na kuboresha maisha na uchumi wa nchi zao. Walimu wameshiriki kwenye tafiti mbalimbali na kupeleka report serikalini, ili kuwezesha uboreshaji wa elimu.
Huku kwetu, serikali yenyewe inawakejeli walimu, inawadharau, inawatukana wakati mwingine na hata kuwadhalilisha. Kwanini tunawashangaa sungusungu ambao hata elimu yao ni ndogo, ili hali hiyo kazi ilianzishwa na viongozi wa ngazi za juu serikalini yaani mkuu wa wilaya? Pamoja ya kwamba alifukuzwa kazi, unafikiri aliacha kitu gani kwa jamii? Pale walimu wanapotangaza mgomo halafu serikali inakimbilia mahakamani na kuuzuia mgomo kwa mabavu, kunatoa heshima gani kwa mwalimu? Mwalimu wa kileo ambaye anapita mitaani kuomba msaada wa chakula na matumizi mbalimbali ya kumsaidia nyumbani kutokana na mshahara mdogo usiotosheleza mahitaji ya nyumbani kwake ataheshimiwa na nani?
Mshahara tunaomlipa mwalimu, ambao unamfanya mwalimu awe na mikopo chungu nzima hapo kijijini anakofanya kazi, kutampa heshima kutoka kwa nani? Ndo maana walimu wengi wa kike huamua kutafuta hifadhi kwa wafanyabiashara humo vijijini: ninayo mifano dhahiri mingi tu. 
Je kwa mfumo wa ualimu wa Tanzania, ukizingatia mtizamo wa serikali kuhusu ualimu na treatment wanazopata kutoka serikalini na kwa jamii, tunaweza kutegemea wawe na uwezo wa kufanya yale ambayo Fullan anasema walimu wanapaswa kufanya? 
Ndiyo maana walimu wa Tanzania wamekuwa kama bendera fuata upepo, hawashirikishwi kwenye maamuzi yanayohusu mabadiliko ya mitaala, badala yake wanapelekewa tu mitaala iliyoamriwa na wenye mamlaka na wao wanafanya kazi ya kuimplement. Na matokeo ya haya ni utoaji wa elimu mbovu, isiyokidhi matakwa na mahitaji ya jamii, pamoja na ongezeko kubwa la udanganyifu katika mitihani. Huu unyanyasaji dhidi ya walimu utaendelea hadi lini? Tunapotaka kulalamika juu ya sungusungu wanachokifanya, tuanze kwanza kuangalia serikali inawafanyia nini walimu. Si ajabu, adhabu ya viboko vya sungusungu ni nafuu kuliko fedhaha wanayoipata ya kufanya kazi ngumu, katika mazingira magumu kwa kipato kiduchu. Na hayo yanafanywa na serikali. Sasa tunataka sungusungu wafanye nini?

No comments: